Mika Chavala logo

Article · 26 July 2026

Maadui Watatu wa Afrika: Kwa Nini Bara Tajiri Linaendelea Kuwa na Mamilioni ya Maskini

Afrika ni miongoni mwa mabara yenye utajiri mkubwa zaidi duniani, lakini mamilioni ya wananchi wake bado wanaishi katika umaskini. Kwa nini? Katika makala hii ya tafakuri na uchambuzi, Mika Chavala anahoji kuwa changamoto kubwa za Afrika si ukosefu wa rasilimali, bali ni maadui watatu wenye nguvu: fikra zilizotawaliwa na ukoloni, uongozi usio na uwajibikaji, na kile anachokiita “ukoloni wa kitaaluma.” Kupitia uchambuzi huu, mwandishi anawahimiza Waafrika kutafakari upya historia yao, kudai uongozi unaowajibika, kuimarisha taasisi, na kukumbatia kujitegemea kama msingi wa ustawi wa kudumu na maendeleo ya kweli ya bara la Afrika.

Maadui Watatu wa Afrika: Kwa Nini Bara Tajiri Linaendelea Kuwa na Mamilioni ya Maskini
“Afrika Itaendelea Kuwa Maskini Ikiwa Tutaendelea Kuagiza Kutoka Nje Vitu Tunavyoweza Kuvizalisha Sisi Wenyewe.”— John Pombe Magufuli

Ni viongozi wachache katika historia ya kisasa ya Afrika waliothubutu kuikosoa kwa uwazi mifumo ya uchumi wa bara hili kama alivyofanya aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli.

Kauli yake haikuhusu biashara au viwanda pekee. Ilikuwa ni changamoto kwa falsafa nzima ya maendeleo ambayo Afrika imeifuata kwa miongo mingi. Kauli hiyo inatulazimisha kujiuliza maswali magumu kuhusu utegemezi, uongozi, elimu na mustakabali wa bara letu.

Kwa nini Afrika inaendelea kuagiza kutoka nje bidhaa ambazo ingeweza kuzizalisha yenyewe? Kwa nini mataifa yaliyojaliwa utajiri mkubwa wa maliasili yanaendelea kutegemea wengine kwa bidhaa za viwandani, teknolojia, na hata chakula?

Na muhimu zaidi, kwa nini bara lenye rasilimali nyingi za asili na watu limeendelea kushindwa kubadilisha uwezo wake mkubwa kuwa ustawi wa kweli kwa wananchi wake?

Maswali haya hayana majibu mepesi. Hata hivyo, tukiamua kuyatazama kwa uaminifu historia yetu na kutathmini mifumo inayotawala jamii zetu leo, tutagundua kuwa changamoto kubwa ya Afrika siyo upungufu wa rasilimali, bali namna tunavyofikiri, namna tunavyoongozwa, na mifumo ambayo tumeruhusu iendelee kuwepo.

Adui wa Kwanza wa Afrika: Akili zilizo na Chembechembe za Ukoloni

Kabla Afrika haijabadilisha uchumi wake, lazima kwanza ibadilishe namna inavyofikiri. Kila ustaarabu mkubwa uliowahi kutokea duniani ulijengwa kwanza katika fikra za watu wake kabla ya kujengwa kwa barabara, viwanda, vyuo vikuu au sekta za uzalishaji. Mataifa hupiga hatua pale wananchi wake wanapoamini kuwa wana uwezo wa kutatua matatizo yao wenyewe. Vivyo hivyo, mataifa huanza kudhoofika pale yanapopoteza imani katika uwezo wao na kuamini kuwa kila suluhisho lazima litoke kwa wengine.

Kwa hiyo, vita kubwa ambayo Afrika inapambana nayo si vita dhidi ya umaskini pekee, bali ni vita dhidi ya fikra ambazo zimehalalisha utegemezi kana kwamba ndiyo hali ya kawaida.

Moja ya sababu zinazochangia hali hii ni namna historia ya Afrika inavyofundishwa. Katika sehemu kubwa ya bara hili, wanafunzi hufundishwa historia ya Afrika kupitia simulizi za utumwa, ukoloni na unyonyaji. Wanatumia miaka mingi kujifunza namna Afrika ilivyotawaliwa na kugawanywa, lakini hutumia muda mfupi sana kujifunza kuhusu ustaarabu uliokuwepo kabla ya ukoloni wa Ulaya.

Historia za Falme za Mali, Songhai, Kush, Axum, Zimbabwe Kubwa, Benin, Ethiopia, Kongo, Buganda na falme nyingine nyingi zilizojenga mifumo ya hali ya juu ya utawala, biashara, elimu, usanifu na diplomasia hazipewi uzito unaostahili.

Kwa nini watoto wengi wa Afrika wanawafahamu vizuri wafalme wa Ulaya kuliko viongozi wa Kiafrika walioongoza dola zenye mafanikio makubwa karne nyingi kabla ya ukoloni?

Kutokuwepo kwa mizani katika simulizi hizi kuna athari kubwa. Jamii inayokuzwa katika historia inayosisitiza kushindwa huanza kujiona kama jamii inayohitaji kuokolewa kila wakati.

Ukweli ni kwamba Afrika ilikuwa kitovu cha maarifa, biashara ya kimataifa, utawala na maendeleo ya kitamaduni muda mrefu kabla ya ukoloni. Kukumbuka historia hii siyo kutukuza yaliyopita, bali ni kurejesha imani kwamba Waafrika wana uwezo wa kujenga mustakabali wao wenyewe.

Mtazamo ndiyo injini ya maendeleo, kila uvumbuzi huanza kama wazo, kila biashara huanza kama maono na kila mapinduzi ya maendeleo ya taifa huanza pale watu wanapoamini kuwa mabadiliko yanawezekana. Iwapo akili za Waafrika zitajikomboa kutoka katika hisia za uduni, utegemezi na hofu, mustakabali wa bara hili utabadilika kwa kiasi kikubwa. Akili iliyojikomboa huzalisha ubunifu, uongozi wenye kujiamini, uvumbuzi na suluhisho za kudumu kwa changamoto za jamii.

Adui wa Pili wa Afrika: Uongozi Usio na Uwajibikaji

Iwapo mtazamo huzaa maono, basi uongozi huamua kama maono hayo yatageuzwa kuwa uhalisia. Afrika si maskini kwa sababu haina utajiri. Ni maskini kwa sababu sehemu kubwa ya utajiri wake haijafanikiwa kuboresha maisha ya wananchi walio wengi.

Bara hili lina baadhi ya akiba kubwa zaidi duniani za dhahabu, almasi, kobalti, lithiamu, mafuta ya petroli, gesi asilia, ardhi yenye rutuba, misitu na vyanzo vya maji safi. Aidha, Afrika ina moja ya idadi kubwa zaidi ya vijana duniani, kundi ambalo ni nguvu kazi na chachu ya maendeleo ya baadaye.

Kila mwaka, serikali za Afrika hukusanya mabilioni ya fedha kupitia kodi, ushuru wa forodha, ada za leseni, mapato yatokanayo na rasilimali za asili pamoja na uwekezaji wa ndani na nje. Wakati huohuo, kampuni nyingi za kimataifa zinaendelea kuwekeza katika sekta za madini, mawasiliano, nishati, kilimo, benki na viwanda kwa sababu zinatambua uwezo mkubwa wa kiuchumi uliopo barani Afrika.

Hata hivyo, licha ya utajiri huo, mamilioni ya Waafrika bado wanakabiliwa na ukosefu wa ajira, huduma duni za afya, miundombinu isiyoridhisha, changamoto za upatikanaji wa umeme wa uhakika, mifumo dhaifu ya elimu na kiwango kidogo cha uzalishaji wa viwandani.

Hapa ndipo swali muhimu linapoibuka:

Ikiwa fedha na rasilimali zipo, kwa nini matokeo hayaonekani?

Hebu tazama bandari za Afrika. Kila siku, meli zinazobeba bidhaa zenye thamani ya mabilioni ya fedha hupita katika bandari za Afrika Kusini, Tanzania, Kenya, Nigeria, Misri, Morocco, Ghana na mataifa mengine mengi. Serikali hupata mapato makubwa kupitia ushuru wa forodha, tozo za bandari, kodi za bidhaa zinazoingia na kutoka nchini pamoja na huduma mbalimbali za usafirishaji.

Zaidi ya hayo, uwekezaji wa moja kwa moja kutoka nje unaendelea kuingia katika sekta mbalimbali za uchumi. Lakini pamoja na shughuli zote hizo za kiuchumi, kwa nini wananchi wengi hawaoni maboresho makubwa katika maisha yao ya kila siku? Hili ndilo swali ambalo Hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliendelea kuwauliza Waafrika mara kwa mara. Kwa mtazamo wake, tatizo kubwa la Afrika halikuwa ukosefu wa rasilimali, bali namna rasilimali hizo zilivyokuwa zikisimamiwa na jinsi fedha za umma zilivyokuwa zikitumika. Mtu anaweza kukubaliana au kutokubaliana na baadhi ya sera zake, lakini hoja hii inastahili kutafakariwa kwa kina.

Maendeleo hayapimwi kwa kiasi cha mapato ambayo serikali hukusanya, bali kwa namna mapato hayo yanavyowekezwa ili kuboresha maisha ya wananchi.

Uongozi wa kweli haupimwi kwa hotuba nzuri wala ahadi nyingi, hupimwa kwa matokeo.

Pale ambapo rasilimali za umma zinajenga shule bora, hospitali za kisasa, miundombinu imara, makazi yanayomudu gharama, viwanda na mazingira yanayowawezesha vijana kuanzisha na kukuza biashara, wananchi huiona na kuigusa maendeleo.

Lakini pale ambapo rasilimali hizo zinapotea kutokana na rushwa, matumizi mabaya ya fedha za umma, uzembe au mipango isiyo na tija, umaskini huendelea kuwepo hata katika nchi zilizojaa utajiri wa maliasili.

Afrika haihitaji viongozi wanaosimamia mamlaka pekee, iInahitaji viongozi wanaosimamia matokeo.

Inahitaji taasisi zinazowajibika kwa wananchi, zinazolinda rasilimali za taifa na kuhakikisha kila senti ya fedha za umma inafanya kazi kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo. Maendeleo ya kweli huanza pale uwajibikaji unapokuwa msingi wa uongozi.

Adui wa Tatu wa Afrika: Ukoloni wa Kitaaluma (Professional Colonialism)

Waafrika wengi huamini kuwa ukoloni ulifikia mwisho mara tu mataifa ya Afrika yalipopata uhuru wa kisiasa katika miaka ya 1960. Ni kweli kuwa uhuru wa kisiasa ulipatikana, lakini unyonyaji haukukoma; ulibadilika tu sura na mbinu zake.

Hali hii ndiyo ninayoita ukoloni wa kitaaluma.

Tofauti na ukoloni wa jadi, ambapo tawala za kigeni zilikuwa zinatawala moja kwa moja ardhi za Afrika, ukoloni wa kitaaluma hufanya kazi kupitia mifumo ya kisheria, kiuchumi na kiutawala inayoruhusu rasilimali za umma na utajiri wa taifa kunufaisha wachache badala ya wananchi wote. Kinachoufanya ukweli huu kuwa mgumu kukubalika ni kwamba mara nyingi wanaonufaika zaidi si wageni, bali Waafrika wenyewe waliopewa dhamana ya kuongoza taasisi na kusimamia mali za umma.

Ni rahisi kulaumu nguvu za nje kwa matatizo ya Afrika. Bila shaka, historia ya ukoloni, siasa za kimataifa na mifumo isiyo sawa ya biashara bado vinaendelea kuathiri maendeleo ya bara hili. Hata hivyo, ni lazima pia tukubali kwamba baadhi ya vikwazo vikubwa vinavyoikwamisha Afrika vinadumishwa na sisi wenyewe. Mara nyingi, wale waliokabidhiwa jukumu la kulinda rasilimali za umma hugeuka kuwa wahusika wakuu wa matumizi mabaya ya rasilimali hizo. Badala ya madaraka kuwa chombo cha kuwatumikia wananchi, hugeuzwa kuwa njia ya kujitajirisha binafsi.

Badala ya taasisi kulinda haki na maslahi ya wananchi, hutumika kulinda maslahi ya kisiasa na makundi machache yenye ushawishi. Fedha ambazo zingejenga shule, hospitali, viwanda, miundombinu na fursa za ajira huishia kunufaisha kundi dogo la watu, huku mamilioni ya wananchi wakiendelea kuishi katika umaskini.

Kwa maana hiyo, ukoloni wa kitaaluma ni mfumo ambao unaruhusu unyonyaji kuendelea chini ya uongozi wa ndani. Hauhitaji tena bendera za kigeni wala majeshi ya kikoloni. Leo, ukoloni unaweza kuonekana katika mikataba isiyo na manufaa kwa taifa, maamuzi yanayowanufaisha wachache, taasisi dhaifu zinazokosa uwajibikaji, na sera zinazoweka maslahi binafsi mbele ya maendeleo ya taifa.

Wakati mwingine huvaa suti za gharama kubwa.

Wakati mwingine huketi kwenye bodi za wakurugenzi.

Wakati mwingine hukaa ndani ya ofisi za serikali.

Na wakati mwingine husaini mikataba ambayo huwatajirisha wachache huku ikiiacha Afrika ikiwa na madeni, utegemezi na maendeleo yasiyokidhi matarajio ya wananchi.

Jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba aina hii ya unyonyaji mara nyingi huonekana kuwa halali kisheria, ilhali matokeo yake hayana tofauti kubwa na yale yaliyotokana na mifumo ya kikoloni ya zamani. Rasilimali Kubwa Zaidi ya Afrika Haipo Chini ya Ardhi—Ipo Ndani ya Akili za Waafrika. Pamoja na changamoto zote hizi, ninaendelea kuwa na matumaini makubwa kuhusu mustakabali wa Afrika. Hakuna bara jingine duniani lenye mchanganyiko wa nguvu kazi ya vijana, utajiri wa maliasili, ubunifu wa watu wake, utofauti wa tamaduni na nafasi ya kimkakati kama Afrika.

Lakini rasilimali kubwa zaidi ya Afrika si dhahabu.

Si mafuta, si almasi, wala si ardhi yenye rutuba, rasilimali kubwa zaidi ya Afrika ni akili ya Mwafrika, ni akili inayoweza kuvumbua. Ni akili inayoweza kutatua changamoto za Afrika kwa suluhisho za Kiafrika, ni akili inayoweza kujenga viwanda badala ya kutegemea bidhaa zinazotoka nje, ni akili inayoweza kuongeza thamani ya malighafi zetu, kuzalisha ajira, kujenga uchumi imara na kuleta maendeleo endelevu.

Hatima ya Afrika haitaamuliwa na kile kilichopo chini ya ardhi yake pekee.

Itaamuliwa na uamuzi wa Waafrika kujikomboa kiakili, kudai uongozi wenye uwajibikaji, kujenga taasisi imara, kuwekeza katika elimu, kuhimiza mapinduzi ya viwanda na kujenga uchumi unaowahudumia wananchi wake kabla ya kuuhudumia ulimwengu. Kama ninavyoeleza katika kitabu changu, Free Minds Build a Free Future, ukombozi wa kweli huanza katika fikra.

Akili huru hukataa utegemezi, akili huru huhoji mifumo iliyoshindwa, akili huru hutafuta suluhisho badala ya visingizio, na pale akili nyingi huru zinapoungana, hujenga jamii huru, taasisi imara na mataifa yenye ustawi.

Afrika haihitaji ruhusa ili iwe tajiri, tayari ina watu, ina rasilimali, ina uwezo. Kinachohitajika sasa ni ujasiri wa kufikiri tofauti, kuongoza tofauti na kujenga tofauti. Siku tutakapofanya hivyo, maneno ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli hayatabaki kuwa onyo, bali yatakuwa msingi wa mapinduzi ya kweli ya kiuchumi ya Afrika.


Free Minds Build a Free Future, kilichoandikwa na Mika Chavala, kinapatikana kupitia Amazon.

Comments

Join the conversation. You can comment anonymously.

Loading comments…